» » TUMAINI LA VIZAZI VYOTE

*_ - Somo la 9_*
🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷🌷
🌷🌷

*SIKU ZA MGONGANO: 1️⃣*

Tangu miaka yake ya mapema mtoto wa Kiyahudi alizungukwa na maagizo ya marabi. Taratibu ngumu 
ziliwekwa kwa ajili ya kila tendo, hata lile lililo dogo kabisa maishani. Chini ya walimu wa sinagogi vijana 
walifundishwa kanuni zisizohesabika amabazo walipaswa kufuata kama Waisraeli wanaoshikilia utamaduni 
wao. 

Lakini Yesu hakujihusisha na mambo hayo. Tangu utoto wake alifanya mambo akiwa huru bila kuongozwa 
na sheria za marabi. Maandiko ya Agano la Kale yalikuwa kitu chake cha kujifunza wakati wote, na maneno, *"Hivi ndivyo asemavyo Bwana,"* yalikuwa midomoni mwake. 

Kadiri hali ya watu ilivyoanza kufunguka katika fahamu zake, aliona kwamba matakwa ya jamii na yale ya Mungu 
yalikuwa katika mgongano wakati wote.

 Watu walikuwa wanaenda mbali na neno la Mungu, na walikuwa 
wakishikilia nadharia walizoibua wenyewe. Waliadhimisha desturi za mapokeo ambazo hazikuwa na uadilifu 
ndani yake. Ibada zao zilikuwa ni mlolongo tu wa kufuata utaratibu; *ukweli mtakatifu ambao ilipangwa kwamba 
ufundishwe kupitia ibada ulifichwa usionekane kwa wanaoabudu.* Aliona kwamba hawakupata amani katika 
ibada zao zisizo za imani. Hawakujua uhuru wa roho ambao ungekuja kwao kwa kumtumikia Mungu katika 
kweli. 

*Yesu alikuwa amekuja kufundisha maana ya kumwabudu Mungu,* na asingeruhusu hali ya kuchanganya 
matakwa ya mwanadamu katika maagizo ya kimbingu. Hakupinga maagizo au ( vitendo vya walimu wale 
wasomi; lakini alipolaumiwa kwa tabia yake ile iliyo nyepesi, *alilitumia neno la Mungu katika kuhalalisha 
mwenendo wake.* 


Katika kila njia ya upole na unyenyekevu, Yesu alijaribu kuwafurahisha wale aliopata kukutana nao. Kwa kuwa 
alikuwa mpole na asiyejitanguliza, waandishi na wazee walidhani kwamba angeweza kushawishiwa na 
mafundisho yao kwa urahisi. Walimtaka apokee kanuni na mapokeo ambayo yalikuwa yamerithishwa kutoka 
kwa marabi wa kale, *lakini alitaka waonyeshe mamlaka ya hayo katika Maandiko Matakatifu.* 

*Angesikiliza kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu;*  lakini hakuweza kutii mavumbuzi ya wanadamu. Ilionekana kama Yesu 
alijua Maandiko kuanzia mwanzo mpaka mwisho, na aliyasema katika umuhimu wake wa kweli. 

*Marabi 
waliaibika kwa kufundishwa na mtoto.* Walidai kwamba ofisi yao ndiyo inayotafsiri Maandiko, na kwamba Yeye 
alistahili kupokea tafsiri yao. Walichukizwa na hali ya Yeye kuwa kinyume na neno lao. 
Walijua kwamba hakuna mamlaka yanayoweza kupatikana katika Maandiko kuunga mkono mapokeo yao. 
Walitambua kwamba Yesu alikuwa mbali sana juu ya wao katika uelewa wa kiroho. Lakini bado walikuwa na 
hasira kwa sababu Yeye hakutii maelekezo yao. 

Wakiwa wameshindwa kumshawishi, walimtafuta Yusufu na 
Mariamu, wakiwaonyesha njia yake ya kutoheshimu. Kwa hiyo alikemewa na kupingwa. 
Katika umri wake wa mapema, *Yesu alikuwa ameanza kutenda kwa kujitegemea katika kutengeneza tabia yake,* 
na hata heshima na upendo kwa wazazi wake havikuweza kumgeuza aache kutii neno la Mungu. *"Imeandikwa"*
ilikuwa ndiyo sababu ya kila tendo ambalo lilitofautiana na desturi za familia. Lakini nguvu ya ushawishi ya 
marabi iliyafanya maisha yake yawe machungu. 

Hata wakati wa ujana wake ilikuwa lazima ajifunze somo gumu 
la kuwa kimya na mvumilivu. 
Kaka zake, walioitwa wana wa Yusufu, walikuwa upande wa msimamo wa marabi. Walisisitiza kwamba lazima 
mapokeo yazingatiwe, kwa kiwango kwamba yalikuwa matakwa ya Mungu. Hata walifikia hatua ya kuyaona 
mafundisho ya wanadamu kama vile yako juu sana kuliko Neno la Mungu, na walichukizwa na maelezo ya wazi 
ya Yesu katika kutofautisha kati ya uongo na ukweli. *Waliuhesabu utii wake kwa sheria ya Mungu kama ukaidi.*
 
*Walishangazwa na ufahamu wake na hekima aliyoonyesha katika kujibu maswali ya marabi.* Walijua kwamba 
hakufundishwa elimu kutoka kwa wenye hekima, *lakini hawakuona kingine bali kama vile alikuwa mwalimu wao.*

 *Waligundua kwamba elimu yake ilikuwa ya juu zaidi kuliko yao.* Lakini hawakukiri kwamba alikuwa na 
uwezo wa kuufikia mti wa uzima, chanzo cha ufahamu ambao hawakuujua. 
*Kristo hakuwa mtu wa kuheshimiwa,* na alikuwa amefanya kosa mahsusi kwa Mafarisayo kwa kule kuachana na 
taratibu zao zisizobadilika. 

Aliona uwanja wa dini ukiwa umezungushiwa wigo kwa kuta zenye kimo kirefu. 
*Alipindua huu ukuta unaotenganisha.* 

Alipokutana na watu hakuuliza, Itikadi yako ya imani ni ipi? Wewe ni wa kanisa gani? 
Alitumia nguvu zake za kusaidia kwa ajili ya wote waliohitaji kusaidiwa.

 Badala ya Yeye kujifungia 
katika chumba cha upweke ili kuonyesha tabia yake ya kimbingu, alitenda kazi kwa ajili ya wanadamu. Alisisitiza 
kanuni ya kwamba dini ya Biblia haiko katika kujitesa mwili. Alifundisha kwamba dini safi isiyo na najisi si ile ya 
kufuata mida iliyopangwa rasmi kwa ajili ya matukio. Alionyesha hamu ya kuwapenda watu wakati wote na 
mahali pote, *na alijivika nuru ya upendo wa kutenda wema.*

 Haya yote yalikuwa ni kemeo kwa Mafarisayo. 
Ilionekana kwake kwamba dini haikuwa katika ubinafsi, na kwamba kuangalia matakwa binafsi ilikuwa ni kuwa 
mbali na uchaji wa Mungu wa kweli. Hali hii ilikuwa imeibua uadui wao dhidi ya Yesu, wakajaribu kumlazimisha 
atii kanuni zao. 

Yesu alifanya kazi ya kuondoa kila namna ya maumivu aliyoona kwa watu. Alikuwa na kiasi kidogo sana cha 
pesa za kutoa, lakini alijinyima chakula ili kuwapatia wale walioonekana kuhitaji chakula zaidi ya vile 
alivyokihitaji. 

Kaka zake waliona kwamba nguvu ya ushawishi wake ilifika mbali na kupita ushawishi wao. 
Alikuwa na uelekevu ambao hakuna mwingine aliyekuwa nao, wala aliyetamani kuwa nao. 

Wakati walipoongea 
na maskini kwa ukali, walipowadhalilisha viumbe, Yesu aliwatafuta hawa hawa, na aliwaambia maneno ya kutia 
moyo. Kwa wale waliokuwa katika uhitaji aliwapa japo kikombe cha maji baridi, na kimya-kimya aliweka 
chakula chake mikononi mwao. Kadiri ambavyo alituliza maumivu yao, ukweli ule aliofundisha uliendana na 
matendo yake ya huruma, na kwa hiyo ulihifadhiwa katika kumbukumbu. 

Haya yote hayakuwafurahisha kaka zake. Wao wakiwa na umri mkubwa kuliko Yesu, walidhani kwamba 
alipaswa awe chini ya maelekezo yao. Walimlaumu kwa kujifanya kuwa juu yao, na walimkemea kwa kujiweka 
juu ya walimu na waandishi na wakuu wa watu. Mara nyingi walimtishia na kujaribu kumshinikiza; lakini 
alisonga mbele, *akiyafanya Maandiko kuwa mwongozo wake.*
 
Yesu aliwapenda kaka zake, na aliwatendea kwa wema mkubwa; lakini walikuwa na wivu kwake, na 
walidhihirisha chuki na kutokuamini kwa wazi mno. Wasingeelewa mwenendo wake. Mgogoro mkubwa uliletwa 
kati yao na Yesu. *Alikuwa Mwana wa Mungu wa asili ya kimbingu,* lakini hapa alikuwa mtoto asiye na wa 
kumsaidia. 

Muumba wa malimwengu, dunia ilikuwa mali yake, lakini umaskini ulikuwa katika kila hatua ya 
uzoefu wa maisha yake. Alikuwa na hadhi na hali ambayo kwa ujumla ilikuwa mbali na fahari ya kidunia na 
kutaka madaraka; hakutafuta ukuu wa duniani, na aliridhika hata katika nafasi ya chini kabisa. Hali hii 
iliwakasirisha kaka zake. Walishindwa kueleza upole wake wa wakati wote hata katika hali ya kujaribiwa na 
kuonewa. Hawakujua kwamba amekuwa maskini kwa ajili yetu, ili ya kwamba tupate *“kuwa matajiri kwa umaskini wake." 2 Wakorintho 8:9.* 

Wangeelewa siri ya utume wake kwa kiasi ambacho si zaidi ya vile ambavyo 
wale rafiki wa Ayubu waliweza kuelewa unyenyekevu na mateso ya Ayubu. 


Yesu hakueleweka vema kwa kaka zake kwa sababu hakuwa kama wao. Kiwango chake hakikuwa kiwango chao. 
Kwa kuwaangalia wanadamu walikuwa wamegeukia mbali na Mungu, na hawakuwa na nguvu zake maishani 
mwao. Kawaida za dini walizoshika hazikuweza kubadili tabia zao. 

Walilipa "zaka za mnanaa na bizari na jira,” 
lakini waliacha *“mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani." Mathayo 23:23.*

 Kielelezo cha Yesu 
kilikuwa kwao jambo la kuchukiza. Alichukia kitu kimoja tu duniani, nacho ni dhambi.

 Hakuweza kushuhudia 
tendo baya bila kuonyesha maumivu yasiyofichika. Tofauti ilionekana wazi kati ya watu walioshikilia dini ya 
mazoea, ambao utakatifu wa kujionyesha ulificha ndani yao kupenda dhambi, na tabia ambayo ilitawaliwa na ari 
ya utukufu wa Mungu. 

Kwa kuwa maisha ya Yesu yalihukumu uovu, alipingwa na makundi yote mawili, la 
nyumbani na la nje ya nyumbani. Uaminifu wake na kutokuwa kwake na ubinafsi vilibezwa.

 Ustahimilivu na 
wema wake vilichukuliwa kama woga. 
Katika sehemu zote za machungu yanayowaangukia wanadamu walio wengi, hakuna ambayo haikuonjwa na 
Yesu. 

Kulikuwa na wale waliojaribu kumtupia lawama kwa misingi ya kuzaliwa kwake, na hata mnamo wakati 
wa utoto wake bado angekutana na kejeli zao na mivumo ya uovu. 

Kama angekabiliana na hayo kwa mtazamo au 
maneno yasiyo na subira, kama angekubaliana na kaka zake hata katika tendo lisilo sahihi, angekuwa 
ameshindwa kuwa kielelezo. Hivyo angekuwa ameshindwa kusonga mbele katika mpango wa ukombozi. 


Angekuwa hata amekubali kuwa na kisingizio cha kukubaliana na dhambi, Shetani angeshinda, na ulimwengu 
ungepotea. 

Hii ndiyo sababu mjaribu aliyafanya maisha yake kuwa ya majaribu kwa kiasi kikubwa 
iwezekanavyo, ili ya kwamba aweze kuanguka.

*_MUNGU BABA TUSAIDIE NA SISI WANA NA BINTI ZAKO TUISHI KULINGANA NA NENO LAKO, NAYE YESU KWETU AWE KIELELEZO CHA UKAMILIFU MAISHANI. AMINA. >>>Itaendelea<<<_*

Pakua App Yetu-Bofya Hapa Flower
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

About 4sn News

Hi my name is Gasto Alex Didas from Mwanza Tanzania I'm blog manager and I have an App which is called 4sn News, my office is located in Rock City Mwanza-Tanzania at Miembeni "B" Street. My contacts +255769436440/ +255659750504 Welcome.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Popular Articles

MBUNGE MABULA AKAGUA SHULE NNE MPYA ZA MSINGI, ZENYE THAMANI YA TSH 1.174 BIL, ASHAURI HALMASHARI KUTUMIA MCHORO MPYA WA TAMISEMI KUOKOA MADARASA 3 KILA SHULE

Mhe. Stanslaus Mabula Mbunge Jimbo La Nyamagana amefanya ziara ya kikazi katika Kata nne za halmashauri ...