Somo la asubuhi Leo Jumanne trh 07/02/2017
Somo:""Hakuna Maswali Yaliyoulizwa"""
Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako. Waebrania 11:8.
Wakazi wa uwanda wa Shinari walijenga ufalme wao kwa ajili ya kujitukuza nafsi, sio kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Kama wangefanikiwa, mamlaka kubwa ingekuwa imechukua madaraka na kuondoa utii wa amri na hivyo kuzinduliwa kwa dini mpya. Dunia ingekuwa imeharibiwa… Lakini kamwe Mungu haachi dunia bila mashahidi wake. Wakati huu kukawa na watu ambao walijinyenyekesha wenyewe mbele za Mungu na kumlilia wakisema, “Ee Mungu, ingilia kati ya kazi yako na mipango na mbinu za watu.”
Wakati mnara ulipokuwa umekamilishwa kwa kiasi fulani, sehemu yake moja ilifanywa kuwa makazi ya wajenzi; vyumba vingine, vikiwa vimenakshiwa kwa uzuri na kupambwa, viliwekwa wakfu kwa sanamu zao….
Ghafla, kazi ambayo ilikuwa ikiendelea kwa mafanikio makubwa ikasimamishwa. Malaika walitumwa ili kufanya kusudi la wajenzi kuwa sifuri. Mnara ulikuwa umefikia kimo cha juu sana na ilikuwa haiwezekani kwa wafanyakazi waliokuwa juu kileleni kuwasiliana moja kwa moja na wale waliokuwa chini kwenye kitako; kwa sababu hiyo, watu waliwekwa kwenye vituo mbalimbali, kila mmoja tayari kupokea na kutoa taarifa kwa yule anayemfuatia chini yake maelekezo kwa ajili ya kitu kilichohitajika au maelekezo mengine yaliyohusu kazi. Ujumbe ulipokuwa ukipita kutoka kwa mmoja kwenda kwa mwingine, lugha ilichanganywa, hivyo kifaa kilichoagizwa sicho kilichohitajika na maelekezo yalifikishwa mara kwa mara sasa yakawa kinyume cha yale yaliyotolewa. Kuchanganyikiwa na fadhaa vikafuata. Kazi yote ikakoma…
Hadi kufikia wakati huo, watu walikuwa wakinena lugha moja; sasa wale walioelewana lugha waliungana kwa makundi; baadhi walikwenda njia moja na wengine nyingine. “Basi Bwana akawatawanya kutoka huko waende usoni pa nchi yote” Kutawanyika huku ilikuwa njia ya kuijaza dunia na kwa namna hiyo kusudi la Bwana lilitimizwa kwa njia ile ile ambayo watu waliitumia kuzuia ukamilishwaji wake. Katika siku zetu, ni shauku ya Bwana kwamba watu wake waenee kote katika nchi. Haiwapasi waanzishe makoloni. Yesu alisema: “Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe” (Marko 16:15).
KARIBUNI
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
No comments:
Post a Comment