YOUNG KILLER: Sinaga Swagga imeua simu yangu
Ni wimbo ambao ndani yake umesheheni mashahiri mengi ya kujikweza na kuwaponda baadhi ya wasanii wenzake wanaoimba Bongo Fleva tena kwa kuwataja majina waziwazi.
Hata video ya wimbo huo ni mwiba pia kwa kuwa ndani kuna vipande kadhaa vinavyoashiria kujikuza kwa msanii huyu kama vile pale anapoonekana akipigiwa simu na supastaa Diamond Platnumz lakini anaikata kwa dharau.
Wimbo huu umeibua mijadala wengi wakajiuliza amefikiria nini pia lipi lengo lake?
Gazeti hili lilimtafuta kuzungumzia wimbo huo.
Chimbuko la Sinaga Swagga
Sinaga Swagga ni wimbo ambao Young Killer aliandika mashairi yake baada ya kuisilikiza ‘beat’. Mwenyewe anaeleza kwamba alichokuwa anahitaji ni kuwashtua mashabiki kwa kutengeneza wimbo ambao hautakuwa wa kucheza lakini utawapa sababu ya kuisikiliza.
Baada ya wimbo kukamilika aliuita ‘Handsome Boy Asiye na Matunzo’ lakini jina hilo halikuwavutia watu wengi ambao aliwasikilizisha wimbo.
“ Kila niliyemsikilizisha aliikubali ngoma lakini jina alilikataa. Nikaona hapa natakiwa kufanya kitu. Nikaamua kutumia Sinaga Swagga kwa sababu ni neno lililotumika kwenye kiitikio na pia ni outro niliyoitumia kwenye ngoma yangu niliyoimba na Juma Nature, inaitwa Popote Kambi,” anaeleza Young Killer.
Sinaga Swagga imepokelewaje?
Mtaani na kwenye mitandao ya kijamii kuna mashabiki wenye mitazamo ya aina mbili tofauti. Wapo wanaosema kwamba wimbo wa Sinaga Swagga ni muendelezo wa kazi nzuri kutoka kwa Young Killer wakati wengine wanaponda juu ya kile alichokiimba.
Anaeleza kwamba kazi yake hiyo mpya imevunja rekodi mbalimbali ikiwemo video yake kupata watazamaji wengi wa Youtube ndani ya muda mfupi ukilinganisha na kazi zake nyingine.
Kuwaponda wenzio vepee?
Majina ya wasanii zaidi ya watatu yamesikika kwenye wimbo huu yakitajwa kwa mtindo wa kuwaponda. Amesikika Young Dee, Dogo Janja, Joh Makini na Billnass.
Kuhusu Joh Makini; Young Killer anaeleza kwamba hakumtaja kama ambavyo watu wengi wamemuelewa, alichokifanya ni kuchukua maoni ya watu wengi mtaani ambao wanadai kwamba Joh Makini anabebwa na akaamua kuyatumia kwenye wimbo wake kama kuwasaidia kufikisha ujumbe kwa mhusika.
Alipoulizwa kuhusu mtazamo wake juu ya kubebwa kwa Joh Makini; Msodoki alisema anamkubali Joh Makini na anaamini anachokifanya ni kizuri na kinaeleweka kwa mashabiki.
Kuhusu Dogo Janja na Young Dee; Young Killer anafafanua kwamba mashabiki wengi wamekuwa wakijitahidi kumlinganisha na Young Dee pamoja na Dogo Janja lakini kwa anavyofahamu ni kwamba ana uwezo mkubwa kuwazidi na ndiyo kwenye wimbo wake akaweka wazi kwamba ‘Hawaogopi na yeye ndiye mkubwa wao wa kazi’.
Kuhusu Diamond; Hakuna sehemu Young Killer anamtaja Diamond Platnumz kwenye ngoma yake isipokuwa kwenye video anaonekana anapigiwa simu na Diamond na anaikata badala ya kupokea. Killer anaeleza kwamba, hilo lilikuwa ni wazo la Director na lengo halikuwa ni Diamond tu, bali walitaka kutumia jina lolote la mtu mkubwa na maarufu Tanzania.
Kuvuka boda je?
Young Killer ni miongoni mwa wasanii ambao hawajasikika wakifanya kazi na msanii kutoka nje ya Tanzania wala kufanya video zao huko. Hata Sinaga Swagga imeendelea kumuweka katika orodha ya wasanii waliofanya kazi ndani tu.
Akijibu kuhusiana na kufanya kazi nje ya Bongo Young Killer alieleza kwamba, wimbo utakaofuata baada ya Sinaga Swagga itakuwa ni kolabo aliyoifanya na msanii wa nje ingawa jina la msanii na nchi anayotoka aliliacha kama ‘Surprise’.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
No comments:
Post a Comment