Wanajeshi wa Kenya kurudi Sudan Kusini
Wanajeshi wa Kenya watajiunga tena na Ujumbe wa kulinda Amani wa Umoja wa Mataifa baada ya kujiondoa mwaka jana kutokana na utata.
Taarifa kutoka Ikulu ya Rais wa Kenya imesema kuwa Umoja wa mataifa pia umekubali kuikabidhi tena Kenya uongozi wa majeshi hao.
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Antonio Guteress walikutana mjini Addis Ababa, Ethiopia ambapo kongamano la Umoja wa Muungano wa Afrika AU linaendelea.
Kulingana na taarifa yake Msemaji wa rais Manoah Esipisu, wawili hAo walikubaliana kurejesha uhusiano mwema ulioko kabla ya Kenya kujiondoa mwezi Novemba mwaka jana.
Umoja wa mataifa ulimtimua Kamanda wa Ujumbe, Luteni Jenerali Johnson Mogoa Ondieki aliye Mkenya, kufuatia ripoti kwamba wanajeshi wa umoja wa mataifa walichelea kuingilia kati huku raia na wafanyikazi wa misaada wakishambuliwa mjini Juba, Sudan Kusini.
Kenya ilisema uamuzi huo haukuwa wa haki na ikaamua kuondoa wanajeshi wake 1500 pamoja na kujiondoa kabisa kwenye shughuli za kutafuta amani nchini humo.
Bwana Guteress alisema amependekeza Kenya ichukue tena uongozi wa wanajeshi hao kama ishara ya imani kwa jeshi la Kenya. Maafisa wakuu wa Umoja wa mataifa na Kenya sasa wataanza majadiliano ya kukirejesha kikosi cha Kenya.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
No comments:
Post a Comment