KESHA LA ASUBUHI
TAREHE 10/10/2016
Tunazaa Matunda Pale tu Tunapokaa Ndani ya Kristo
▶Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Yohana 15:4.
▶Sababu inayofanya tuwe wazembe katika maisha ndani ya dhambi ni kwamba hatumwoni Yesu. Tusingechukulia dhambi kwa urahisi kama tungeutambua ukweli kwamba dhambi inamuumiza Bwana wetu… Tathmini sahihi ya tabia ya Mungu ingetuwezesha kumwakilisha yeye kwa usahihi duniani. Ukali, fujo katika kunena au tabia, kunena uovu, maneno ya mhemko, haviwezi kuwepo ndani ya nafsi ambayo inamwangalia Yesu. Yeye akaaye ndani ya Kristo yumo kwenye angahewa linalokataza uovu na hatoi udhuru hata uwe mdogo kiasi gani kwa ajili ya jambo lolote la namna hiyo. Maisha ya kiroho hayanawirishwi kutokea ndani, bali huchukua lishe yake kutoka kwa Kristo, kama tawi lifanyavyo kutoka kwenye mzabibu. Tunamtegemea Kristo kila wakati; yeye ndiye hazina ya mahitaji yetu. Namna zetu zote zinazoonekana nje, maombi, kufunga na utoaji wa sadaka haviwezi kuchukua nafasi ya kazi ya ndani ya Roho wa Mungu kwenye moyo wa mtu.
▶Mtu anapokuwa ameacha ubinafsi, wakati kila mungu wa uongo anapokuwa ameondolewa moyoni, ombwe hilo hujazwa na Roho wa Kristo anayetiririkia ndani. Mtu wa namna hiyo anakuwa na imani inayotakasa moyo toka katika uchafu… Yeye ni tawi la Mzabibu wa Kweli na atazaa vishada vilivyosheheni matunda kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Tunda linalozaliwa lina tabia gani? – Tunda la Roho ni “upendo,” siyo chuki; “furaha,” siyo kutoridhika na kuomboleza; “amani,” siyo kero, fadhaa na majaribu ya kutengeneza. Ni “uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi.”
▶Hakuna tawi linaloazima riziki yake kutoka kwa lingine. Uzima wetu lazima utoke kwenye mzabibu –mkuu uliotuzaa. Ni kwa umoja binafsi pamoja na Kristo tu, kwa kuwasiliana naye kila siku, kila saa, tunaweza kuzaa matunda ya Roho Mtakatifu…. Ukuaji wetu katika neema, furaha yetu, utumikaji wetu, vyote vinategemea umoja wetu na Kristo na kiwango cha imani tuliyonayo katika yeye.

No comments:
Post a Comment