Yanga kumalizana na Mwadui
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Yanga leo watakuwa wenyeji wa Mwadui katika mchezo wa ligi utakaochezwa uwanja Taifa, Dar es Salaam.
Mara ya mwisho timu hizo zilikutana Septemba mwaka jana mjini Shinyanga katika mchezo wa raundi ya kwanza ambapo Yanga ilishinda mabao 2-0 yakifungwa na Amis Tambwe na Donald Ngoma.
Mchezo wa leo una umuhimu kwa kila mmoja kushinda Yanga ikitaka kuwa karibu na Simba kwa ajili ya kutetea taji lake na Mwadui ambao bado hawako katika nafasi nzuri wakihitaji pointi kujiweka sehemu salama.
Lakini Yanga inapewa nafasi kubwa ya kushinda mchezo huo ikijivunia kuwa na kikosi bora kinachonolewa na Kocha Mkuu George Lwandamina na msaidizi wake Juma Mwambusi. Aidha, Mwadui inayonolewa na Kocha Ally Bushir ‘Bush’ina kazi kubwa ya kuhakikisha inapata pointi tatu ili kujiweka sehemu salama zaidi.
Kwa sasa Mwadui inashika nafasi ya 11 ikiwa na pointi 22 na Yanga ikiwa na pointi 45 katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Simba.
Yanga itaendelea kumkosa mchezaji wake tegemeo Donald Ngoma ambaye yupo kwao kwa matatizo ya kifamilia.
Kocha Msaidizi wa Yanga Juma Mwambusi alisema wako tayari kwa mapambano kuhakikisha wanashinda mechi zote kwasababu wanataka kutetea taji.
“Tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri, wachezaji wote wako tayari kwa mchezo. Tunaifahamu Mwadui sio timu rahisi wana wachezaji wazuri na wengine baadhi waliwahi kucheza Yanga, kwa hiyo utakuwa ni mchezo mgumu,”alisema.
Mechi nyingine itakayochezwa leo ni Majimaji ya Songea dhidi ya Ndanda kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.
Timu zote mbili haziko vizuri huku Majimaji ikishika nafasi ya pili kutoka mwisho kwa pointi 17 na Ndanda FC ikishika nafasi ya 13 ikiwa na pointi 19. Kila mmoja anahitaji ushindi kuondoka kwenye hatari ya kushuka daraja.
CHANZO HABARI LEO
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
No comments:
Post a Comment