» » Kanisa lapiga marufuku ndoa wanawake waliozaa

KANISA la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), limepiga marufuku kuanzia sasa ufungishaji ndoa madhabahuni kwa wanawake waliozaa.



Aidha, kanisa hilo ambalo ni moja ya mawili makubwa zaidi nchini limepiga marufuku pia wanawake wenye ujauzito kufunga ndoa madhababuni kwa maelezo kuwa kufanya hivyo ni kiuka maandiko ya Mungu.

Kutokana na uamuzi huo wa Kanisa, kuanzia sasa wanawake wenye sifa hizo hawataruhusiwa kukaa mbele ya madhabahuni na kufunga ndoa wakiwa wamevaa shela.

Badala yake, imeelezwa, ndoa zinazohusu wanawake maharusi wa namna hiyo zitafungwa katikati ya ibada ya kawaida; wakiwa wamekaa na waumini wengine.

Ni kawaida makanisani sasa kuona wanawake wakifunga ndoa wakiwa ama walishazaa watoto baada ya kuishi na mwanaume kinyumba hapo kabla, au wakiwa na ujauzito madhabahuni.

Kanisa hilo limesema wanawake waliozaa au kuwa na ujauzito watatakiwa kufanya tendo la kubariki ndoa bila kuvaa shela jeupe.

Kwa mujibu wa tangazo lililosomwa katika sharika mbalimbali za KKKT Jumapili iliyopita, ni marufuku wachungaji kuendelea kufungisha ndoa kwa waumini ambao wameshazaa na badala yake wabariki ndoa yao.

Nipashe imefuatilia kanuni na taratibu za kanisa hilo na kugundua haziruhusu mwanaume kufungishwa ndoa na mwanawake mwenye ujauzito au aliyezaa.

Alipoulizwa ufafanuzi juu ya tangazo hilo, Mkuu wa Jimbo la Kaskazini la KKKT, Dayosisi ya Mashariki na Pwani, mchungaji Anta Muro hakukubali wala kukataa kutangazwa kwake badala yake alimuomba mwandishi kuwasiliana na gazeti la Upendo linalomilikiwa na kanisa hilo.

Hata hivyo, mmoja wa maofisa katika Makao Makuu ya KKKT jijini Dar es Salaam, alilieleza Nipashe kuwa tangazo hilo lilitolewa ikiwa ni sehemu ya kuwakumbusha waumini warudi kwenye kanuni na sheria za kanisa.

“Ilikuwa ni kuwakumbusha waumini tu warudi kwenye mstari kwa sababu hizi ni kama sheria za kanisa hili kuwa mwanamke ambaye amezaa bila ndoa anatakiwa arudishwe kundini baada ya hapo ndipo abariki ndoa yake na mwenza wake,” alisema.

Alieleza kuwa hata suala la shela jeupe kwa wanawake ni vazi ambalo linatakiwa kuvaliwa na wanandoa ambao hawajawahi kuishi pamoja na kwamba mambo kama hayo kuzungumziwa kanisani ni kama kukumbushana.

Aidha, mtumishi huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini kwa kuwa si msemaji alisema baadhi ya wachungaji wamekuwa wakisahau au kutembea nje ya sheria za kanisa, "kwa kufuata taratibu za kidunia ambako watu huamua kuishi kiholela na kuzaa kama siyo Wakristo walioishi na kulelewa kwenye imani.”

Katika makanisa kadhaa ya KKKT waumini pia wamekumbushwa kuwa kitendo cha mwanamke kushika kwanza ujauzito ni jambo ambalo halikubaliki na binti kama huyo anatakiwa kurudishwa kwanza kundini ndipo abariki ndoa.

“Kuanzia sasa tunasisitiza kuwa kanisa halitamfungisha ndoa mwanamke ambaye tayari amezaa au amebeba ujauzito kama mnavyotaka, isipokuwa tutamrudisha kundini kama mwenye dhambi na baadaye tutaibariki ndoa hiyo katikati ya ibada,” ilitangazwa ibadani katika Mtaa wa Neema, Usharika wa Mbezi Luis wiki iliypita.

Ilieleza zaidi kuwa jambo hilo limekuwa kama mazoea kwa vijana na mabinti kufanya uzinifu kwanza kabla ya kufunga ndoa na baadaye kuamua kwenda kanisani.

Mchungaji wa KKKT Usharika wa Kigogo, Richard Hananja, alisema jambo hilo siyo jipya kwa kanisa hilo bali limetangazwa kama sehemu ya kuwakumbusha waumini.

Alisema waumini ambao wameshazaa au kuishi wote hurudishwa kwanza kundini kabla ya kubariki ndoa hiyo na kwamba kama kuna baadhi ya makanisa yametangaza basi ni suala la kukumbushana.

“Ingawa mi siamini sana katika kuendelea kuwapa masharti waumini ambao tayari wameshaamua kutubu na kurudishwa kundini kwa sababu waumini wengi huanza kwanza mahusiano kabla ya ndoa,” alisema.

UKUAJI WA TEKNOLOJIA
Mchungaji Hananja alisema kutokana na mfumo wa maisha ya sasa na ukuaji wa teknolojia, vijana wengi huanza uhusiano kabla ya ndoa hali ambayo husababisha wanapofikia maamuzi ya kufunga ndoa kuwa walishazaa tayari.

Alishauri kanisa kuendelea kutoa elimu makanisani na kuwakumbusha vijana wajibu wao ndani ili waweze kuishi katika misingi ya kuzishika amri za Mungu.

Baadhi ya waumini wa kanisa hilo walisifia hatua hiyo na kusema kuwa itasaidia kupunguza tabia ya vijana kuendekeza kuanza maisha kabla ya ndoa.

Johnson Massawe, muumini wa kanisa hilo, alisema hatua hiyo ina faida mbele za Mungu na itasaidia mabinti kutokimbilia kwa wanaume kabla ya ndoa.

Alisema kwa upande mwingine ni fedheha kwa sababu itamuumiza mwenye binti aliyeshindwa kufungishwa ndoa na badala yake akabariki kwa sababu tu alishazaa au kubeba ujauzito.

“Hili ni jambo jema linatusaidia Wakristo kutambua wajibu wetu na kurudi kwenye mstari ambao tunatakiwa tuwepo badala ya kuishi maisha tunayoyataka sisi," alisema Massawe.

"Siyo watu wote watapenda kusikia habari kama hii, lakini ndiyo ukweli wenyewe.”

Riziki Munishi alisema jambo hilo linaleta nidhamu makanisani na kwamba waliokuwa wakichangia vijana kufunga ndoa wakiwa na ujauzito ni wachungaji.

“Ni jambo jema, lakini tatizo wachungaji hawakulisimamia tangu mwanzo kama ndugu zetu walokole (ambao) wao ni misimamo isiyobadilika," alisema Munishi.

"Huku kwetu wanatoka nje ya mstari na kurudi kama ni sheria za kanisa basi ifahamike hivyo na kila mtu aziheshimu.”

Jenipher Alawi, alisema suala hilo litawafanya ambao tayari wana ujauzito kuogopa kwenda kanisani kubariki ndoa na matokeo yake kuishia kuishi maisha ya dhambi.

“Kwa wale ambao hawajafanya hivyo itawasaidia, lakini hawa ambao tayari wameshaingia kwenye dhambi kama hii itasababisha wasije kabisa kanisani na kuendelea na dhambi hiyo,” alisema Alawi.

KUKIUKA KANUNI
Kwa upande wake kiongozi wa Kanisa la Pentekoste nchini, Askofu Emanuel Mwamalanga, akizungumza na Nipashe juzi alisema kufungisha ndoa mwanamke akiwa mjamzito au ameshazaa ni kukiuka kanuni na taratibu za makanisa mengi nchini.

Alisema miongoni mwa mambo ambayo makanisa mengi ya Wakristo yanazuia kwa watu wanaotaka kufungishwa ndoa ni pamoja na kuzaa.

“Kanisa haliruhusiwi kabisa kumfungisha ndoa mwanamke ambaye ana ujauzito wa mwanaume mwingine au hata kama umempa wewe unayetaka kumuoa,” alisema.

Mwamalanga alisema ndoa nyingi zinavurugu kwa sababu zinafungwa kwa kutofuata misingi ya ndoa za Kikristo.

Akizungumzia vazi jeupe ambalo mara nyingi huvaliwa na bibi harusi, alisema maana yake ni usafi wa moyo na ishara ya kumuheshimu Mungu.

Kuhusu ndoa ya serikali, alisema mtu haruhusiwi kuvaa shela kwa sababu ni ndoa ya sheria ya mwili na haitambuliki mbele za Mungu bali kiserikali.

Pakua App Yetu-Bofya Hapa Flower
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

About 4sn News

Hi my name is Gasto Alex Didas from Mwanza Tanzania I'm blog manager and I have an App which is called 4sn News, my office is located in Rock City Mwanza-Tanzania at Miembeni "B" Street. My contacts +255769436440/ +255659750504 Welcome.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Popular Articles

MBUNGE MABULA AKAGUA SHULE NNE MPYA ZA MSINGI, ZENYE THAMANI YA TSH 1.174 BIL, ASHAURI HALMASHARI KUTUMIA MCHORO MPYA WA TAMISEMI KUOKOA MADARASA 3 KILA SHULE

Mhe. Stanslaus Mabula Mbunge Jimbo La Nyamagana amefanya ziara ya kikazi katika Kata nne za halmashauri ...